Friday, March 4, 2016

ZAIDI YA ASILIMIA 60 YA MAKAO YA WATOTO HAYAJASAJILIWA.

 Mkuruenzi Mtendaji, Joel Kiiya akizungumza na waandishi habari katika mkutano wa tano wa Ninajali  ulioshirikisha wadau mbalimbali juu ya malezi mbadala ya mtoto uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Afisa wa Taifa wa Jinsia,Catherine Kazimbazi waandishi habari katika mkutano wa tano wa Ninajali  ulioshirikisha wadau mbalimbali juu ya malezi mbadala ya mtoto uliofanyika jijini Dar es Salaam.
Picha ya pamoja ya wadau wa taasisi zinazojishughulisha utetezi wa watoto walipokutana katika mkutano wa Ninajali Media Dialogue uliofanyika jijini Dar es Dar es Salaam.

Na Chalila Kibuda,Globu ya Jamii
 ZAIDI ya asilimia 60 ya makao ya watoto Tanzania hayajasajiliwa huku zaidi ya 80% ya makao haya yanamilikiwa na watu/mashirika binafsi. Hii ilionekana katika Mdahalo wa Nijali uliofanyika jijini Dar es Salaam leo.
Mdahalo huu uliandaliwa na wadau mbalimbali wa masuala ya watoto nchini pamoja na waandishi wa habari, maafisa ustawi wa jamii kutoka Hai, Temeke na Iringa pamoja na Idara ya Ustawi wa Jamii.
 
Akizungumza katika mkutano huo Mkurugenzi Mtendaji  wa C-sema, Joel Kiiya amesema mkutano ulikuwa unaangalia  hali ya Malezi Mbadala kwa watoto nchini.
 
Msimamzi  wa kituo cha Huduma ya Simu kwa Mtoto (116),Fatma Kamramba amesema kuwa walikutana na  kesi  moja ilionekana kuwa katika baadhi ya makao, watoto hufanyiwa ukatili.
 
Nae Msimamizi wa Kituo cha simu,Thelma Dhaje, , alielezea kesi  ya mvulana wa miaka 13 aliyekuwa akilawitiwa na msimamizi/mmiliki wa kituo kimoja cha watoto Dar es Salaam.
 
 “Kuna watoto wengi wanaohitaji makao ya kudumu au ya muda wakiwemo watoto wale walioko mitaani, waliosafirishwa kiharamu na wanaofanyiwa ukatili nyumbani. Makazi ya watoto yanatakiwa kuwa salama na watoto wapelekwe katika makazi haya pale tu panapokosekana sehemu nyingine salama kwa ajili yao,” amesema . Dhaje.
 
Kwa mujibu wa sheria, makao yoyote ya watoto yanatakiwa kuwa yamesajiliwa na Idara ya Ustawi wa Jamii kabla ya kuanza kupokea watoto. Hata hivyo, ilionekana kuwa bado makao mengi ya watoto hayajasajiliwa rasmi na huendeshwa chini ya kiwango kinachotakiwa.

Kuna jitihada mbalimbali zinazofanywa na serikali nchini ili kuhakikisha watoto waliopo katika mazingira hatarishi wanapata malezi mbadala na makao salama. Hata hivyo, bado kuna upungufu wa makazi haya. “Kati ya changamoto kubwa tulizo nazo ni upungufu wa makao ya watoto yanayomilikiwa na serikali,” amesema  Sango Omari, Afisa Ustawi wa Jamii kutoka wilaya ya Hai. Bi. Sango alieleza kua upungufu wa makao haya unasababishwa na mapato madogo katika ngazi za wilaya ambayo huzorotesha mfumo mzima wa ulinzi na usalama wa mtoto.
 
Mwaka 2009, Umoja wa Mataifa walitoa Muongozo wa Malezi Mbadala ya Watoto ili kuboresha mfumo wa ulinzi na usalama wa mtoto na utekelezaji wa Mkataba wa Haki za Mtoto (CRC). Muongozo huu upo kwa ajili ya kuwalinda watoto ambao wamekosa malezi ya wazazi au wako katika mazingira hatarishi.

Kampeni ya Nijali ambayo imekua ikiendelea kwa mwaka mmoja ni muendelezo wa Kampeni ya Shirika la SOS duniani iitwayo “Care for Me!” na hufadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Austria (Austrian Development Cooperation). Midahalo hii hukusudia kuhimiza utengaji na utekelezaji wa bajeti kwa masuala ya watoto na kuhakikisha kua Idara ya Ustawi wa Jamii imewezeshwa kushughulikia afya, elimu na maslahi ya mtoto kwa ujumla. Kampeni hii inatumia midahalo ili huduma za watoto Tanzania bara na visiwani ziweze kuboreshwa kuanzia ngazi ya serikali za mitaa.
Kuhusu C-Sema

C-Sema inataka kuona huduma za watoto nchini zinalenga maslahi ya mtoto. Kwa kushirikiana na serikali ya Jamuhuri wa Muungano wa Tanzania, C-Sema inakusanya maoni ya watoto nchi nzima kupitia Huduma ya Simu kwa Mtoto (116), Barua za Maoni ya Watoto, na gazeti la Sema kwa ajili ya watoto. Maoni haya hutumiwa na viongozi wa manispaa katika kuongeza bajeti ya watoto ili kuboresha huduma za watoto.

Kuhusu SOS Children’s Villages Tanzania
Tunawawezesha watoto wanaohitaji malezi ya kifamilia ili waweze kufanikisha malengo yao maishani.

Tunawapa nafasi kuishi katika familia na kujenga mahusiano ya kudumu na familia hizi, huku tukitilia mkazo tamaduni na dini za anakotoka. Tunawapa fursa za kupata elimu na ujuzi wa kuwasaidia kuwa na nyenzo muhimu za mafanikio maishani.

No comments: