Tuesday, March 8, 2016

TANZANIA NA JAPAN KUANZISHA USHIRIKIANO KATIKA MATUMIZI YA TEHAMA.

Mwakilishi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA) nchini Tanzania Bw. Toshio Nagase akimweleza jambo Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Faustin Kamuzora (kushoto).
Mwakilishi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA) nchini Tanzania Bw. Toshio Nagase (kulia) akizungumza na baadhi ya watendaji wa Wizara hiyo upande wa Mawasiliano wakiongozwa na Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Faustin Kamuzora.
 Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Faustin Kamuzora (kushoto) akisisitiza jambo alipokutana na  Mwakilishi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA) nchini Tanzania Bw. Toshio Nagase. Bw. Toshio Nagase amekutana na kufanya mazungumzo na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo kuhusu namna Japan na Tanzania zinavyoweza kushirikiana katika masula ya TEHAMA.
Picha na Aron Msigwa –MAELEZO

Na. Aron Msigwa –MAELEZO
TANZANIA na Japan zinatarajia kuanzisha ushirikiano katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa kuwaunganisha wafanyabishara na vijana wanaojihusisha na masuala ya TEHAMA ili waweze kunufaika na fursa zilizopo katika nchi hizo.

Hayo yamebainishwa leo jijini Dar es salaam na Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof. Faustin Kamuzora mara baada ya kukutana na kufanya mazungumzo na Mwakilishi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Maendeleo la Japan (JICA) nchini Tanzania Bw. Toshio Nagase ambaye alimtembelea ofisini kwake kueleza nia ya Shirika lake na nchi ya Japan kutaka kuwekeza kwenye Sekta ya TEHAMA nchini Tanzania.

Amesema mara baada ya kukamilika kwa taratibu zote za ushirikiano katika sekta ya TEHAMA vijana na wafanyabishara wa Tanzania wataweza kushirikiana na vijana na wafanyabiashara kutoka Japan katika kubadilishana uzoefu na ujuzi katika masuala ya TEHAMA na kuwawezesha kujiajiri wenyewe au kuajiriwa ndani na nje ya nchi.

Prof. Kamuzora amesema  kuwa Tanzania na Japan kwa muda mrefu zimekuwa zikishirikiana katika masuala mbalimbali ya maendeleo kupitia miradi ya ushirikiano  hususan ujenzi wa miundombinu na masuala ya Ufundi.

Aidha, amesema kuwa Tanzania imekuwa ni nchi ya kuigwa duniani na kupigiwa mfano kwa kuwawezesha wananchi kupata huduma ya kutuma na kupokea pesa kupitia simu za mkononi na kufanya malipo mbalimbali.

“sisi kama Serikali tunawakaribisha wenzetu wa Japan kuja Tanzania kushirikiana nasi kuendeleza Sekta ya Mawasiliano na kuwekeza nchini kwetu ili wananchi wetu wanufaike na maendeleo ya Sekta hii kama ambavyo wenzetu wamepiga hatua kwa kuwa na kampuni za vifaa vya TEHAMA kama vile kampuni ya Sony”. Amesema Prof. Kamuzora.

Amesisitiza kuwa Serikali ya awamu ya tano chini ya uongozi wa Rais John Magufuli imeweka msisitizo katika uanzishaji na uendelezaji wa viwanda kwa lengo la kukuza ajira miongoni mwa watanzania na kuongeza kuwa mkakati uliopo ni kuanzisha viwanda vya kuzalisha vifaa mbalimbali vya TEHAMA kwa kuwa Soko bidhaa hizo lipo.

Ameongeza kuwa Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na JICA imejipanga kuwekeza katika Elimu,Ujuzi na Stadi kwa vijana ili waweze  kutengeneza Program za TEHAMA ambazo zinahitajika ndani na nje ya nchi hivyo kukuza uchumi miongoni mwa vijana hao.

Kuhusu kuwekeza katika Elimu katika masuala ya TEHAMA Prof. Kamuzora amesisitiza kuwa hakuna nchi iliyowahi kuendelea duniani bila kuwa na wabunifu wake wa ndani na kuongeza kuwa Tanzania sasa inao vijana wenye uwezo wanaofanya vizuri katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.

“Dhana ya kutengeneza viwanda lazima ihusishe ubunifu wa kutengeneza Programu, hakuna nchi iliyoendelea bila kuwa na wabunifu wa ndani tunachohitaji sasa ni uwepo wa vijana ambao wakao tayari ” Amesisitiza Prof. Kamuzora.

Prof. Kamuzora amesema Tanzania inazo fursa nyingi za kuwawezesha vijana ikiwemo uanzishaji wa viwanda vidogo na vya kati vya kutengeneza programu za TEHAMA hivyo ushirikiano ulioonyeshwa na JICA utawezesha  viwanda vya kutengeneza vifaa mbalimbali kuanzishwa kupitia wabunifu waliopo.
 “ Tanzania tunao vijana wabunifu wenye uwezo, kupitia Tume ya Sayansi na Teknolojia ( COSTECH) wameweza kubuni na kutengeneza teknolojia mbalimbali  kusaidia shughuli za Kilimo na uhifadhi wa Maliasili hapa nchini” Amesema.

Aidha, amesema Wizara kwa kushirikiana na JICA inafanya mpango wa kuwakutanisha wafanyabiashara; wawekezaji; kampuni; sekta binafsi na wadau mbalimbali wa Sekta ya Mawasiliano wa Tanzania na Japan ili kubadilishana uzoefu na kuainisha fursa na maeneo ya kushirikiana kwa lengo la kuendeleza sekta hiyo na ushirikiano wa nchi hizo mbili kwenye Nyanja ya TEHAMA.

Kwa upande wake mwakilishi Mkuu wa JICA nchini Tanzania Bw. Toshio Nagase akizungumza mara baada ya kufanyika kwa mazungumzo hayo amesema kuwa Tanzania na Japan kwa miaka mingi zimekuwa na ushirikiano wa karibu katika masuala mbalimbali.

Ameipongeza Tanzania kwa kupiga hatua na kufanya vizuri katika matumizi ya TEHAMA kwenye huduma za fedha kwa njia ya Simu na kubainisha kuwa Japan inayo mengi ya kujifunza kupitia mafanikio haya.

Amesma JICA imejipanga kusaidia awamu ya pili ya program zao nchini Tanzania hususan kwenye Miundombinu, uwekezaji kwenye TEHAMA na masuala ya kiufundi katika maeneo mbalimbali ambayo miradi ya ushirikiano inatekelezwa.
Nagase ameeleza kuwa Japan imejipanga kushirikiana kikamilifu katika masuala ya TEHAMA hususan kuwawezesha vijana na wafanyabiashara wa Tanzania na Japan kubadilishana uzoefu, ujuzi, ufundi katika masuala ya TEHAMA.

Amebainisha kuwa Japan iko tayari kushirikiana na Sekta binafsi nchini Tanzania kupitia biashara na uwekezaji kwenye makampuni yanayojishughulisha na TEHAMA.

No comments: