Thursday, February 18, 2016

Kwaya mbili kusindikiza Tamasha la Pasaka.

Na Mwandishi Wetu
KWAYA mbili za nyimbo za Injili zimethibitisha kushiriki Tamasha la Pasaka linalotarajia kufanyika mikoa ya Kanda ya Ziwa kuanzia Machi 26 hadi 28.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Kamati ya maandalizi ya tamasha hilo, Alex Msama tamasha hilo linaanza Geita katika ukumbi wa Desire ambalo litafanyika Machi 26, Mwanza kwenye uwanja wa CCM Kirumba litafanyika Machi 27 na Kahama Machi 28 kwenye uwanja wa Taifa.

Msama alizitaja kwaya hizo zinazotarajia kupanda jukwaani katika mikoa hiyo ni pamoja na AIC Makongoro Vijana ya jijini Mwanza sambamba na Wakorintho Wapili ya Mafinga ya Iringa.

Msama alitoa wito kwa wakazi wa mikoa hiyo kujitokeza kwa wingi katika tamasha hilo ambalo malengo yake ni kusaidia wenye uhitaji maalum ambao ni walemavu, yatima na wajane.

“Nawaomba wakazi wa mikoa ya Kanda ya ziwa kujitokeza kwa wingi ili tuwasaidie wenzetu wenye uhitaji maalum ambao ili wafikie malengo wanahitaji kutoka kwetu,” alisema Msama.

Aidha Msama alisema bado wanaendelea kufanya mawasiliano na waimbaji mbalimbali wa Tanzania ambao kwa pamoja watafikisha ujumbe wa neno la Mungu kwa jamii.

No comments: