Tuesday, July 21, 2015

MAMA SALMA KIKWETE AHUDHURIA MKUTANO WA 9 WA WAKE WA MARAIS KUHUSU KANSA HUKO NAIROBI...

 
Mke wa Rais Mama Salma Kikwete akielekea kwenye ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Jomo Kenyetta huko Nairobi kuhudhuria mkutano wa 9 wa Wake wa Marais wa Nchi za Afrika unaozungumzia magonjwa ya saratani ya matiti, shingo ya kizazi na tezi dume tarehe 20.7.2015.
Baadhi ya wajumbe kutoka Tanzania wanaoshiriki kwenye mkutano wa 9 wa Wake wa Marais wa Afrika wakifuatilia kwa makini sherehe za ufunguzi.
Mke wa Rais Mama Salma Kikwete na Mke wa Rais wa Niger Madame Dkt. Lalla Malika Issofou Mahammadou wakiwa kwenye sherehe za ufunguzi wa mkutano wa 9 wa Wake wa Marais wa nchi za Afrika. Mkutano huo ulifunguliwa rasmi na Rais wa Kenya Mheshimiwa Uhuru Kenyetta (hayupo pichani) tarehe 20.7.2015.
Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya na wake wa Marais kutoka nchi mbalimbali barani Afrika wamesimama wakati wimbo wa Taifa wa Kenya ukiimbwa.
Rais Uhuru Kenyatta wa Kenya akiwa amesimama na baadhi ya wake wa Marais wa Afrika wakati wimbo wa Mataifa ya Afrika ukiimbwa. Kushoto kwa Rais Kenyatta ni Mkewe Mama Margret Kenyatta akifuatiwa na Mke wa Rais wa Namibia Mama Monica Geingos, Mama Salma Kikwete na mwisho ni Mama Dkt. Lalla Malika Issofou Mahammadou wa Niger.
Baadhi ya Wake wa Marais wa Nchi za Afrika wakishiriki kumvisha mkanda maalum kwa kuteuliwa kwake kuwa Balozi wa Hiari kwenye Masuala ya Afya ya Mama na Mtoto Barani Afrika. Wanaomvisha mkanda huo kwa niaba ya wake wa Marais ni (kutoka kushoto kwenda kulia) Princess Nikky Onyeri, Mwanzilishi na Mkurugenzi Mkuu wa ‘Forum of African First Ladies against Cervical, Breast and Prostate Cancer, Mama Dkt. Lalla Mahammadou wa Niger, Mama Monica Geingos wa Namibia, Mama Mary Ayen Mayardit wa Sudan Kusini. Mama Salma Kikwete na Mwisho ni Mama Mathato Mosisili wa Lesotho.
Mke wa Rais Mama Salma Kikwete akiteta jambo na Princess Nikky Onyeri, Mwanzilishi wa Forum of African First Ladies Against Cervical, Breast and Prostate cancer mara baada ya viongozi hao kutembelea Hospitali ya HH Aga Khan jijini Nairobi tarehe 20.7.2015.PICHA NA JOHN LUKUWI 

Na Anna Nkinda – Nairobi, Kenya
Asillimia 70 ya wagonjwa wa saratani hupoteza maisha katika nchi zinazoendelea na katika Bara la Afrika lenye watu zaidi ya milioni 804 asilimia  12.4 wanapata saratani kabla ya kufikia umri wa miaka 75  na asilimia  90 wanapata ugonjwa huo wakiwa na  umri wa chini ya miaka 40.

Hayo yamesemwa na Rais wa Kenya Mhe. Uhuru Kenyatta wakati akifungua mkutano wa tisa wa Jukwaa la wake wa marais wa Afrika la kutokomeza magonjwa ya saratani za mfumo wa uzazi ambazo ni mlango wa kizazi, matiti na tezi dume unaofanyika katika ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Kenyatta (KICC) uliopo mjini Nairobi.

Rais Kenyatta alisema Ripoti ya saratani iliyotolewa mwaka 2014 na  Shirika la Kimataifa la kutafiti saratani kwa kushirikiana na Shirika la Afya Duniani (WHO) ilionyesha takwimu mpya za saratani zinaongezeka  kila mwaka na kwa upande wa Afrika  vifo vingi vinatokana na saratani ya mlango wa kizazi.

“Watu wanapoteza maisha na kuugua saratani kutokana na kutokuwa na uelewa wa ugonjwa huo, kutokuchukua hatua za mapema na watu kutambulika  kuwa na ugonjwa wa saratani wakati umefikia hatua ya mwisho kutokana na hili tutaendelea kuwa na wagonjwa ambao wanapata maumivu, wanashindwa kupata matibabu kwa wakati na  uangalizi wa karibu katika bara letu”. 

Ni lazima tuhakikishe jamii inajulishwa kuhusu ugonjwa wa saratani na  kubadilisha aina ya maisha tunayoishi kama watu wataacha kuvuta sigara, watakula vyakula vyenye afya, atapunguza kunywa pombe na kufanya mazoezi mara kwa mara tutakuwa tumezuia asilimia 40 ya saratani”, alisema.

Aidha Mhe. Rais Kenyatta alisema katika bara la Afrika ugonjwa wa saratani siyo moja ya agenda inayopewa kipaumbele katika masuala ya afya ukilinganisha na magonjwa mengine kama ya  kuambukiza  lakini sasa ili kupambana na saratani kunatakiwa kuwa na mikakati kwa nchi chache ambazo zitaweza kukutana na  kufanya utafiti na kutoa matibabu ili kuzuia watu wasife na hivyo kuokoa maisha katika hatua ya mwanzo ya ugonjwa.

Mhe. Rais Kenyatta alimalizia kwa kusisitiza kuwa watu wanahitaji kupata chanjo ya hepatitis ambayo inazuia saratani ya  Ini na  Human Papilloma Virus (HPV) inayozuia saratani ya mlango wa kizazi ambazo zitasaidia kupunguza idadi ya saratani katika bara la Afrika.

Akiwakaribisha wake wa marais na wadau mbalimbali wa afya  waliohudhuria mkutano huo Mke wa Rais wa Kenya Mhe. Mama Margaret Kenyatta alisema ni muhimu wadau hao wakaendelea kushirikiana na kufanya kazi  kwa pamoja ili kukabiliana na magonjwa hayo ya saratani.

Mhe. Mama Kenyata ambaye ni Mwenyekiti mpya wa Jukwaa la wake wa marais wa Afrika la kutokomeza magonjwa ya saratani za mfumo wa uzazi ambazo ni mlango wa kizazi, matiti na tezi dume kwa mwaka 2015 – 16 alisema wamefanikiwa kuongeza uelewa kwa jamii kuhusu magonjwa ya saratani wanachotakiwa kukifanya hivi sasa ni  kuendelea kuhamasisha jamii ili waweze kujichunguza dalili za awali za saratani na kutibiwa kuzuia kwani saratani nyingi zikigundulika mapema zinatibika.

Alisisitiza, “Tunatakiwa kuwashawishi viongozi, Serikali na sekta binafsi na taasisi zisizo za kiserikali kuchukua hatua za lazima ili kuweza kukabiliana na saratani na hivyo kuokoa maisha ya watu wetu”.

Kuhusu ulaji wa vyakula alihimiza ni muhimu waafrika wakaangalia maisha ya zamani na kurudi nyuma kwa  kuanza kula vyakula vya asili na kuacha  kula vyakula vilivyosindikwa  hasa kwa vijana”


Mkutano huo wa siku tatu wenye kauli mbiu ya wekeza kuokoa maisha: wajibu wa ushirikiano wa sekta binafsi ulihuhuriwa na wake wa Marais kutoka nchi 12 akiwemo Mke wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Mama Salma Kikwete.

No comments: