Saturday, April 11, 2015

ACT YATIKISA SONGEA.





















MJI wa Songea jana ulizizima kwa mapokezi makubwa  ya viongozi wa  Chama cha ACT-Wazalendo wakiongozwa na kiongozi wa chama hicho Zitto Kabwe.
Zitto, ambaye ameambatana na viongozi wengine wa juu wa ACT akiwemo Mwenyekiti wa ACT Taifa, Anna Mghwira pamoja na Katibu Mkuu wake Samson Mwigamba.
Viongosi hao walisili jana mjini hapa  ambapo walilakiwa na mamia ya wananchi wa mji wa Songea wakiongozwa na vijana wa bodaboda zaidi ya 300.
Akihutubia mamia ya wananchi jana mjini Songea katika mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye Uwanja wa Stendi ya Malori Majengo, Zitto, alisema lengo la kuanza ziara mkoani Ruvuma ikiwa kuenzi na kutekelza kwa vitendo azimo la Songea.
Alisema na hilo pia mkoa huo una historia ya ukombozi wa vita ya majimaji iliyoanzia wilayani Kilwa na baadaye kuenea hadi Songea.
Mbunge huyo wa zamani ya Kigoma Kaskazini, alisema kutokana na hali hiyo ACT-Wazalendo wameanza ziara hiyo ili kupata baraka za mababu wa ukombozi na si kushindana au kuviponda vyama vingine vya siasa.
Alisema kitendo cha baadhi ya watu kufikiri kuwa ziara yake ina lengo la mashambulizi si sahihi bali sasa ni changamoto kwa wakazi wa mkoa wa Ruvuma kuhakikisha wanapanda viongozi wa upinzani kama njia ya kustawisha demokrasia nchini.
“Ruvuma ni Mkoa ambao hauna mbunge wa upinzani hata mmoja na tumeona tutume salamu kwa umma huku lengo letu likiwa likiwa kuing’oa CCM madarakani na kwamba hatuna nia ya kugambana na vyama vingine.
“Wakazi wa Songea ni wajibu wenu kupima je pamoja na historia ya ukombozi ambayo ACT-Wazalenzo tunaamini ndio misingi ya ukombozi wan chi yetu je kukosa mbunge hata mmoja wa upinzani ni sahihi, hili ni lazima tulikate na tufanye uamuzi huo sasa hasa kuelekea Oktoba mwaka huu,” alisema Zitto.
Akizungumzia Mkoa wa Ruvuma kama mmoja wa mikoa mitano inayotegemewa kwa uzalishaji mkubwa wa chakula, alisema pamoja na wakulima kuhangaika usiku na mchana lakini bado hakuna juhusu za Serikali za kuwakomboa katika lindi la umaskini ili wafurahie kilimo chao.
Alisema kwa muda sasa bei za mazao zimekuwa zikishuka lakini bado Serikali imeshindwa kuwalipa wakulima Sh bilioni 13 za mahindi bila kuwa na utaratibu madhubuti wa kulipa madeni hayo.
“Kwan chi zilizoendelea zimekuwa zikithamini juhudi zinazofanywa na wakulima ikiwemo kuundiwa mfuko wa mazao, ambao unafanya kazi ya kuhakikisha dhamani ya mazao inalindwa.
“Ikitoa bei ya mazao inashuka linakua jukumu la mfuko  kulipa fidia ya hasara kwa wakulima, ambapo hili huenda sambamba na kuwepo kwa mfuko huo ambao.
“Nasi ACT- Wazalendo tungependa kuonyesha sera yetu ya hifadhi ya jamii ambapo kila mkulima awe na bima ya afya. Mpango wetu ni kwamba kama mchango wa hifadhi ya jamii ni Sh 30,000 basi Serikali itamchangia mkulima Sh 10,000,” alisema Zitto
Alisema kutokana na changamoto za wakulima wanataka kuonyesha wana majawabu ambapo mkulima atatibiwa bure akiwa na hifadhi ya jamii na uhakika wa bei kupitia mfumuko wa bei katika hifadhi ya jamii.
“Utafiti wa Shirikala la Kazi Duniani (ILO), wa mwaka 2013 unaonyesha kuwa nchi ambazo zimesambaza hiafdhi ya jamii kwa wananchi wake wote zimeondoka kwenye umaskini kwa kasi na ukiaji wa uchumi unaongezeka mara dufu,” alisema Kiongozi huyo wa ACT-Wazalendo
Mgomo wa madereva
Mbunge huyo wa zamani wa Kigoma Kaskazini, alisema kuwa kilichotokea jana ni mapambano kati ya wenye nguvu na wanyonge kwani madereva hawana mikataba ya kazi zao lakini wamiliki wamekuwa wakiwanyonya madereva huku Serikali iksihindwa kuchukua hatua zozote.
“Hatua za kuimarisha usalama lazima ziendane na usalama wa ajira za Watanzania katika sekta ya usafirishaji hivyo Serikali ichukue hatua za haraka kwa kukutana na viongozi wa madereva na kupata suluhisho la kudumu.
“Waziri Samuel Sitta asitishe kwa muda uamuzi wa Serikali kuhusu mafunzo na Serikali ihakikishe madereva wote wana mikataba ikiwemo michango kwenye hifadhi ya jamii, Serikali itekeleze uamuzi wa mafunzo.
“Kuna haja ya kuhakikisha kuwa udereva wa mabasi ya abiria ni taaluma hivyo kuwepo na mfumo wa ‘accredition’ kupitia umoja wa madereva katika usafirishaji wa umma,” alisema
Zitto alisema ACT-Wazalendo, inasimama upande wa wanyonge hivyo ipo na madereva wote nchini wanaovuja jasho kuzalisha kwa ajili ya matajiri wao na pia tunaitaka Serikali imalize tataizo hili mara moja na wananchi waendelee na shughuli za uzalishaji kama kawaida.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa ACT-Wazalendo, Anna Mghwira, alisema chama chake hakina ugomvi na chama chochote cha siasa nchini na kipo tayari kushirikiana na chama kinachoamini katika itikadi za kitaifa.
“Ninajua hapa kuna watu wamekuwa wakisema kuwa ACT-Wazalendo haitaki kushirikiana na vyama vingine hili si kweli kubwa tunachosema kama kuna chama kinaamini katika misingi ya ujamaa kije tutashirikiana nao,” alisema Anna.
Kabla yakuwahutubia wananchi mjini hapa viongozi hao wa ACT-Wazalendo, alisema wakazi wa vitongoji vya mji huo Zitto alifungua matawi kadhaa ya chama hicho ambapo alielezea mikakati ya chama hicho kuelekea Uchaguzi Mkuu unaotarajiwa kufanyika Oktoba mwaka huu.
Matawi yaliyofunguliwa jana katika eneo la Mshangano, Bombambili, Msamala kwa Mauki na Lizaboni.
Mbali na kufanya shughuli hizo pia walitembelea makumbusho ya mashujaa mjini hapa pamoja na kufanya vikao na viongozi wa chama wa ngazi ya mkoa kama njia ya kujiimarisha.

No comments: