Sunday, June 14, 2015

MAELFU YA WANANCHI WA HALMASHAURI TATU ZA MKOA WA MORO WANUFAIKA NAMPANGO WA MKURABITA.

 Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dk.Rajabu Rutengwe kushoto akifurahia jambo na Mratibu wa Mkurabita Saraphia Mgembe.
 Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Dk.Rajabu Rutengwe mwenye suti nyeusi akiongoza kucheza ngoma ya Sangula ya wapogolo baada ya kuzindua utoaji wa hati miliki za kimila chini ya Mkurabita wilayani Kilombero.
Baadhi ya wananchi mbalimbali wa wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro wakimsiliza Mkuu wa Mkoa wa Morogoro .
 Furaha ya hati ya miliki za kimila na Mkurabita.
  Baadhi ya wananchi mbalimbali wa wilaya ya Kilombero Mkoani Morogoro wakiwa katika picha ya pamoja.

Na John Nditi, Morogoro
WAKUU wa wilaya  , Wakurugenzi  na Wenyeviti wa halmashauri ambazo  zimenufaikana Mpango  wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara  za Wanyonge Tanzania ( MKURABITA), wametakiwa kuitumia  fursa hiyo adhimu kuwapatia wananchi wao maendeleo kwa kutumia rasilimali ardhi katika kukuza uchumi wa taifa letu. 

Rai hiyo imetolewa na Mratibu wa Mkuratiba nchini, Saraphia Mgembe, Juni 10, mwaka huu mjini Ifakara wakati  wa uzinduzi wa kimkoa wa utoaji wa hati miliki za kimila kwa baadhi ya wananchi wa halmashauri ya wilaya ya Kilombero,  ambao mgeni rasmi alikuwa mkuu wa mkoa huo, Dk Rajab Rutengwe.

Pamoja na hayo  alisema ,katika kupambana na upungufu wa fedha, Mkurabita imejiandaa kufanya majaribio ya kuunda Mfuko wa Urasimishaji utakaoendeshwa kwa mfumo wa dhamana.

Kwa mujibu wa Mratibu hiyo kuwa, utekelezaji wa urasimishaji ardhi mijini uliofanyika katika  Manispaa ya Morogoro umetoa  hamasa ya kuujaribu mfuko wa urasimishaji kutokana na uzoefu uliopatikana katika  Manispaa hiyo.

Hata hivyo alisema katika mpango huo kwa mkoa wa Morogoro ni  halmashauri  wilaya tatu  ya Kilosa, Mvomero na Kilombero  zimenufaika kwa urasimishaji wa ardhi vijijini na  jumla mashamba  9,180 yamepimwa na yameandaliwa hati za hatimiliki za kimila  7,837.

Pia alisema , Mkurabita umeendesha zoezi la urasimishaji ardhi mijini katika Manispaa ya Morogoro kwenye  Kata ya Mbuyuni, Mlimani, Lukobe na Kihonda  ambapo idadi ya wamiliki 222 walichangia uzalishaji wa viwanja 1,122 na hati 72 zimeandaliwa ambapo Manispaa itaendelea kurasimisha mitaa mingine na kuzalisha viwanja vingine 5,660.

Hivyo alitoa rai  kwa wananchi walionufaika na mpango huo wazitumie  hati hizo katika kujikwamua na umaskini kwa kupata mikopo na mitaji kutoka taasisi zetu za fedha na mabenki.

Mbali na hayo, aliwataka Wakurugenzi wa halmashauri ambazo kazi ya urasimishaji imefanyika sasa waiendeleze kazi hoyo kwa kuhakikisha watendaji wao wanafanya kazi kwa uadilifu mkubwa .

“ Tunapofika hatua hii watu wengi hawatofaitishi maofisa wa Mkurabita na wale wa halmashauri wanapokosa uadilifu ‘vitendo vya rushwa’ wananchi husema ni Mkurabita , wananchi mnapoona utata wowote toeni taarifa ili maamuzi stahiki kwa watumishi wasiowaadilifu “ alisema Mratibu huyo.

Naye Mkuu wa mkoa wa Morogoro, Dk Rutengwe, katika hotuba yake ya uzinduzi alisema hati hizo hazina ukomo wake,  ni dhamana ambayo taasisi za fedha zinazitambua na hivyo wananchi walirasimishwa wanapata  fursa ya mikopo na mitaji ya kujiendeleza.

Hata hivyo alisema, hati za kimika zina manufaa makubwa kwa wananchi kwa kusaidia  kuinua uchumi wao , kuimarisha usalama wa miliki ya ardhi na dhamana ya kupata mitaji ya mikipo itakayoongeza uboreshaji wa shughuli za uzalishaji ili kujiongezea kipato.

“  Nawasihi wananchi wote mliopokea hati hizi mzitumie kwa manufaa yenu na kuboresha maisha na si nyaraka za kuficha na kuhifadhi tu” alisema Mkuu wa Mkoa.

Hata hivyo pamoja na kuupongeza Mkurabita , mkuu huyo wa mkoa aliomba mpango huo uendeleze kujenga uwezo katika halmashauri zilizobakia ya Gairo, Ulanga na Halmashauri ya wilaya ya Morogoro.

No comments: