Wednesday, June 17, 2015

BASATA LAWATAKA WASANII KUWA TAYARI KUKOSOLEWA.

Na Mwandishi Wetu 

 Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limetoa wito kwa wasanii kuacha tabia ya kulewa umaarufu na kuchukia pale wanapokosolewa kwani kazi yoyote ya Sanaa lazima ikosolewe ili iwe bora na yenye kuvutia. 

 Wito huo umetolewa mapema wiki hii na Katibu Mtendaji wa Baraza hilo Godfrey Lebejo Mngereza wakati akizungumza kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA linalofanyika kwa mwezi mara mbili siku ya Jumatatu kwenye Ukumbi wa Baraza hilo ulioko Ilala Sharif Shamba jijini Dar es Salaam.

 Alisema kuwa wasanii wafurahie wanapokosolewa kwani msanii yeyote duniani lazima atenge muda wa kuiwasilisha kazi yake kwa hadhira kwa ajili ya kusikilizwa au kuangaliwa na hatimaye kukosolewa na kutolewa mawazo ya wadau kabla haijaenda sokoni rasmi. “Kukosolewa kwa msanii ni sehemu ya kazi. 

Wasanii wengine hulipa fedha nyingi kwa ajili ya kukosolewa na kuboreshewa kazi zao. Hapa kwetu wasanii wanakosolewa bure, wanakasirika, wanamwona adui anayewakosoa” aliongeza Lebejo.

 Awali wakiwasilisha mada iliyohusu Umuhimu wa msanii kutumia umaarufu kukuza pato kwa nyakati tofauti kwenye Jukwaa hilo, mbunifu wa mavazi maarufu nchini Asia Idarous and mwanamitindo Jokate Mwegelo kwa pamoja walisisitiza umuhimu wa wasanii kuwa na malengo, bidii, uaminifu na kutengeneza kazi zenye ubora. 

 Jokate alisema kwamba amefika hapo alipo kutokana na kuzingatia uhusiano mwema katika kazi, kujitangaza, kujituma, kujiwekea akiba na kujenga mtandao mzuri wa kikazi na wadau mbalimbali ndani na nje ya nchi pia kujenga umaarufu mzuri usiyo na maadili mabovu. 

 “Kupata umaarufu si kwa mteremko. Si kila umaarufu ni mzuri. Wasanii lazima wabuni kazi nzuri na zenye maadili ili zionekane na kupendwa. Tusibuni vitu vibaya au sisi wenyewe kujinadi kwa vitu vibaya” alisisitiza Jokate. Alizidi kueleza kwamba hakuna kitu cha muhimu kwa msanii kama uvumilivu , kuepuka makundi yasiyo na tija na zaidi kuwa karibu na watu wenye mafanikio katika kazi zao ili kuiga yale yaliyo bora kwa ajili ya kukuza uchumi na pato.
Msanii na mwanamitindo Jokate Mwegelo (Kushoto) akiongea na wadau wa Jukwaa la Sanaa la Baraza la Sanaa la Taifa-BASATA (hawako pichani) mapema wiki hii kwenye ukumbi wa Baraza hilo ulioko Ilala Sharif Shamba jijini Dar es Salaam. Wengine kutoka kulia ni Mbunifu wa mavazi maarufu nchini Asia Idarous na Katibu wa Chama cha Waandishi wa habari za Sanaa na Utamaduni (CAJAtz), Hassan Bumbuli.
Mbunifu wa mavazi maarufu nchini Asia Idarous (Kulia) akisisitiza jambo mapema wiki hii wakati akiwasilisha mada kwenye Jukwaa la Sanaa la Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) katika Ukumbi wa Baraza hilo ulioko Ilala Sharf Shamba jijini Dar es Salaam. Wengine katika picha kutoka kushoto ni Mwanamitindo Jokate Mwegelo na Katibu wa CAJAtz Hassan Bumbuli.
Katibu Mtendaji wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) Godfrey Lebejo akipiga marimba ya kigogo mapema wiki hii kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA linalofanyika kila Jumatatu mara mbili kwa mwezi kwenye ukumbi wa Baraza hilo ulioko Ilala Sharif Shamba jijini Dar es Salaam. Wanaoshuhudia kushoto kwake ni Mwanamitindo Jokate Mwegelo, Katibu wa CAJAtz Hassan Bumbuli na mbunifu mavazi Asia Idaorus.
Katibu wa Chama cha Waandishi wa habari za Sanaa na Utamaduni (CAJAtz) Hassan Bumbuli (Katikati) akisisitiza jambo mbele ya wadau wa Sanaa (hawako pichani) kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA linalofanyika mara mbili kwa mwezi siku ya Jumatatu kwenye Ukumbi wa Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) ulioko Ilala Sharif Shamba. Kulia ni Mbunifu mavazi Asia Idarous na mwanamitindo Jokate Mwegelo.
Msanii mkongwe wa Sanaa za majukwaani nchini Kasim Mbelemba maarufu kama Mzee Jangala (Mwenye bhalagashia) akifuatilia kwa makini mjadala kwenye Jukwaa la Sanaa la BASATA mapema wiki hii.
Mdau wa Sanaa akichangia mada kwenye Jukwaa la Sanaa mapema wiki hii huku baadhi ya wadau wakisikiliza ka makini.
Sehemu ya wadau wa Sanaa waliohudhuria programu ya Jukwaa la Sanaa mapema wiki wiki kwenye Ukumbi wa BASATA ulioko Ilala Sharif Shamba jijini Dar es Salaam.

No comments: