Thursday, May 7, 2015

E-FM 93.7 RADIO STATION NA MICHUZI BLOG ZA UNGANISHA NGUVU KUNOGESHA LIBENEKE LA MICHEZO, MUZIKI NA UTAMADUNI



Mwenyekiti Mtendaji wa Michuzi Media Group  (MMG) Ankal Muhidin Issa Michuzi (kulia) na Meneja Maslahi na Sheria wa Kituo cha redio cha 93.7 E-Fm Bw. Denis Ssebo  wakipeana mikono baada ya  kusaini mkataba wa makubaliano ya ushirikiano  kwenye hafla fupi zilizofanyika Jumatano Mei 6, 2015 kwenye ofisi za kituo hicho cha redio Mikocheni jijini Dar es salaam.


Pamoja na mambo mengine MMG na Kituo cha redio cha 93.7 E-FM kuanzia sasa watashirikiana katika mambo ya habari, matangazo na shughuli zingine za kijamii ikiwa ni pamoja na michezo, muziki na utamaduni.
“Hii ni siku ya kihistoria katika tasnia ya habari nchini Tanzania kwa makubaliano haya ya kwanza ya aina yake ambapo kituo chetu cha 93.7 E-FM kilicho mstari wa mbele kukuza tasnia za michezo, muziki na utamaduni wa Tanzania na MMG inayoendesha na kuongoza katika tasnia ya habari mtandanoni nchini ya Michuzi Blog pamoja na Michuzi online TV kukubaliana kufanya kazi pamoja.

“Hii ni baada ya kila upande kugundua  kwamba ina wapenzi lukuki ndani na nje ya Tanzania kuliko vyombo takriban vyote vya habari Tanzania, na pia kwa pamoja kuona haja ya kuenzi na kukuza tasnia za michezo, muziki na utamaduni wa Tanzania ambavyo pamoja na umuhimu wake vyombo vingi vya habari havijazipa tasnia hizo msukumo wa kutosha.
“Hivyo sisi kwa pamoja tumeamua kuungana na kufanya mabadiliko makubwa kwenye kuendeleza tasnia za michezo, muziki na utamaduni kwa nguvu zetu zote”, alisema Bw. Ssebo.

Kwa pande wake, Ankal, ambaye anaamini katika vitendo zaidi ya kuongea, alisema MMG inayoendesha Michuzi Blog a.k.a Globu ya Jamii, pamoja na Michuzi TV online, watafanya kile ambacho wengi hawafanyi ama kama wanafanya inakuwa kijuu juu tu.

“93.7 E-FM radio station imedhihirisha ndani ya mwaka mmoja tu kwamba michezo, utamaduni na jamii ya Tanzania vinaweza kupendwa na kuthaminiwa na kila mtu ndani nan je ya Tanzania…
“Kwa kuwa Ubunifu, kujituma na juu ya yote kuwapa wananchi kile roho zao zinapenda ni dira ya MMG na kituo hiki cha redio kinachokuja juu kwa kasi ya ajabu na kustua, wadau wetu wakae mkao wa kula kila siku kwani maneno hayavunji mfupa”alisema Ankal, ambaye blog yake pendwa kuliko zote nchini ya Michuzi Blog mwaka huu inatimiza miaka 10  ya kuanzishwa kwake.

Kituo cha redio cha 93.7 E-FM kina mwaka mmoja tu toka kuanzishwa kwake lakini kimetokea kuwa kituo pendwa nchini Tanzania kwa kuenzi tasnia za michezo, muziki na utamaduni, wakati Globu ya Jamii inatajwa kuwa ndiyo Blog ya Kiswahili inayosomwa zaidi duniani.

No comments: