Makamu
wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad na Balozi
mdogo wa China aliyepo Zanzibar Bw. Xie Yun Liang, wakifurahi baada ya
kukata utepe kuashiria ufunguzi rasmi wa kitengo cha wagonjwa mahututi
(ICU), katika hospitali ya Mnazi Mmoja.
Makamu
wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad akitembelea
wodi mpya ya wagonjwa mahututi (ICU), katika hospitali ya Mnazi Mmoja,
baada ya kuifungua rasmi.
Baadhi
ya wanafunzi wa chuo cha afya Mbweni, wakiwa sehemu ya washiriki katika
hafla ya ufunguzi wa wodi ya wagonjwa mahututi katika hospitali ya
Mnazi mmoja.
Makamu
wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad,
akisisitiza jambo wakati wa ufunguzi wa kitengo cha wagonjwa mahututi
(ICU), katika hospitali ya Mnazi Mmoja.
Katibu
Mkuu Wizara ya Afya Dr. Mohamed Saleh Jidawi, akizungumza wakati wa
ufunguzi wa kitengo cha wagonjwa mahututi (ICU), katika hospitali ya
Mnazi Mmoja.
Makamu
wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad, akigana
na Balozi mdogo wa China aliyepo Zanzibar Bw. Xie Yun Liang, baada ya
kumalizika hafla ya ufunguzi wa kitengo cha wagonjwa mahututi (ICU),
katika hospitali ya Mnazi Mmoja. Wa pili kulia ni Waziri wa Afya Mhe.
Rashid Seif Suleiman. (Picha na Salmin Said, OMKR)
Na: Hassan Hamad, OMKR
Makamu
wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Maalim Seif Sharif Hamad,
amewasisitiza wananchi kufuata taratibu na maelekezo ya hospitali, ili
kuwawekea wagonjwa mazingira bora.
Maalim
Seif ametoa kauli hiyo katika hafla ya ufunguzi wa kitengo cha wagonjwa
mahututi (ICU) cha hospitali kuu ya Mnazi Mmoja, ikiwa ni shamra shamra
za maadhimisho ya miaka 51 na Mapinduzi ya Zanzibar.
Amesema
wagonjwa hasa wanaotibiwa katika wodi ya wagonjwa mahututi wanahitaji
utulivu na uangalizi maalum, hivyo hakuna budi kwa wananchi kwa
watendaji wa hospitali na wananchi kuwawekea mazingira bora kwa ajili ya
matibabu yao.
Amesema
iwapo wananchi watashindwa kufuata taratibu hizo ambazo zimewekwa kwa
lengo la kuweka mazingira bora ya hospitali, wanaweza kusababisha
usumbufu na athari zisizokuwa za ulazima kwa wagonjwa, ikiwa ni pamoja
na kuwasababishia matatizo mengine ya kiafya.
Sambamba
na hilo Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar amewahimiza wafanyakazi wa
hospitali kuwa wapole na wavumilivu wakati wote, ili kuwapa matumaini
wagonjwa na wananchi wanaofika hospitali kwa ajili ya kupatiwa huduma.
Amesema
kumekuwepo na malalamiko ya muda mrefu kwa wafanyakazi wa hospitali
kutokuwa na lugha nzuri wakati wanapowahudumia wagonjwa, jambo ambalo
linakiuka maadili ya taaluma ya afya.
Amesema
wakati umefika kwa wafanyakazi hao kubadilika ili kulinda heshima ya
taaluma hiyo na kujenga matumaini mapya kwa wagonjwa wanaofika
hospitali.
“Kitendo
cha kumjali mgonjwa ikiwa ni pamoja na kumpa lugha nzuri ni sehemu ya
matibabu kwa mgonjwa huyo, na hapo hapo anaweza kujisikia kuwa amepata
nafuu kutokana mapokezi mazuri aliyoyapata. Kwa hivyo watendaji wa afya
mnatakiwa kuwa na nyuso za tabasamu wakati wote mnapowahudumia
wagonjwa”, alitanabahisha Maalim Seif.
Maalim
Seif amewatahadharisha watendaji wa sekta ya afya kuacha kuhatarisha
maisha ya watu kwa sababu ya kushindwa kuchangia gharama za matibabu.
Amesema
kitu cha msingi ni kuweka mazingira ya kujaribu kuokoa maisha ya
mgonjwa kwanza, na gharama za matibabu zinaweza kujadiliwa baada ya
mgonjwa kupata nafuu.
Hata
hivyo Maalim Seif ameelezea kuridhishwa kwake na hali nzuri ya wodi hiyo
mpya ya wagonjwa mahututi, na kuelezea matumaini yake kuwa itatunzwa na
kuendelezwa.
Amesema
kuwepo kwa wodi hiyo yenye vitendea kazi vya kisasa katika hospitali ya
mnazi mmoja, kutasaidia kupunguza gharama za matibabu kwa wagonjwa
waliokuwa wakisafirishwa nje ya Zanzibar kutafuta huduma hiyo.
Aidha
Maalim Seif ameitaka Wizara ya Afya kuweka mkazo katika utoaji wa
mafunzo na kuwaendeleza vijana katika taaluma ya afya, ili kupunguza
tatizo la wataalamu wa sekta hiyo.
Mapema
akizungumza katika hafla hiyo, Waziri wa Afya Mhe. Rashid Seif
Suleiman, amesema serikali inajitahidi kupata vifaa vya kisasa vya
uchunguzi, ili kuwawezesha madaktari kufanya kazi zao kwa uhakika.
Amesema
katika kuimarisha sekta ya afya, Wizara hiyo ina mpango wa kupata dawa
kwa ajili ya matumizi ya Zanzibar bila ya kupita muda wake wa matumizi,
sambamba na kujenga wodi mpya ya akinamama wanaokwenda kujifungua katika
hospitali hiyo.
Nae
Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Dr. Mohamed Saleh Jidawi, amesema lengo la
kujengwa kwa wodi hiyo mpya ni pamoja na kuinua afya za wananchi pamoja
na kuokoa maisha yao.
Amefahamisha
kuwa wodi hiyo sasa imeimarika kwa kuwa na vifaa vyote vinavyohitajika
kwa ajili ya uchunguzi na upimaji, na kwamba hatua hiyo itaondosha
tatizo la wagonjwa hao kupelekwa sehemu nyengine kwa uchunguzi.
Wodi
hiyo yenye vitanda vinane na vifaa vya uchunguzi, imetengenezwa kwa
mashirikiano katika Serikali ya China na Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar, na imegharimu dola milioni moja nukta mbili hadi kukamilika
kwake.
No comments:
Post a Comment